Monday, October 28, 2013

VIONGOZI CHADEMA WAZIPIGA KAVUKAVU

Mkutano wa Baraza la Uongozi la Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Kanda ya Kaskazini juzi uligeuka ukumbi wa ngumi, baada ya Mwenyekiti wa chama hicho Mkoa wa Arusha, Samson Mwigamba kushushiwa kipigo.

Mwigamba alishushiwa kipigo hicho na baadhi ya viongozi wenzake wa chama kwa madai ya usaliti na tayari amesimamishwa uongozi kwa muda usiojulikana.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Liberatus Sabas jana alithibitisha kutokea kwa vurugu hizo na viongozi hao wa Chadema kufikishana polisi.

Alikutwa na zahama hiyo mbele ya viongozi wakuu wa Chadema Taifa, Mwenyekiti, Freeman Mbowe na mwasisi wa chama hicho, Edwin Mtei katika Hoteli ya Coridal Spring.

Viongozi hao wamekuwa wakifanya ziara za aina hiyo nchi nzima, kuimarisha chama na kujipanga kwa ajili ya uchaguzi wa Serikali za Mitaa mwakani na uchaguzi mkuu ujao wa Rais na wabunge mwaka 2015.

Habari kutoka ndani ya mkutano huo zinaeleza kuwa hatua hiyo ilifuatia tuhuma kwamba Mwigamba alitumaujumbe kwenye mtandao wa kijamii wa Jamii Forums, unaodaiwa kukichafua chama hicho.


Tukio hilo la aina yake lilitokea wakati viongozi wote wa juu wa chama hicho, wakiongozwa na Mbowe walipokuwa wakijadili mustakabali wa chama hicho, mkutano ambao ulihudhuriwa na wabunge karibu wote wa Chadema wa kanda hiyo.


Hata hivyo, wakati mijadala ikiendelea baadhi ya viongozi wa chama hicho, akiwamo Mbunge wa Jimbo la Arusha Mjini, Godbless Lema walimtuhumu Mwigamba kutuma ujumbe kwenye mtandao huo, uliokuwa ukizungumzia ufisadi ndani ya chama hicho, wakidai alitaka Mwenyekiti Mbowe kukubali kuchunguzwa.


Akizungumza na Mwananchi Jumapili jana, Mwigamba alisema kuwa baada ya Lema kutoa tuhuma hizo aliungwa mkono na viongozi wengine na vijana waliokuwa wameimarisha ulinzi, kumvamia na kuanza kumpiga pamoja na kumnyang’anya kwa nguvu kompyuta mpakato (Laptop), aliyokuwa nayo, kisha kumpeleka Kituo Kikuu cha Polisi, mjini Arusha.


“Wamenipiga sana na kuniweka ndani, ila nashukuru Mkuu wa Upelelezi wa Wilaya ya Arusha (OCCID), alikuja na kunitoa saa 5:00 asubuhi,” alisema Mwigamba.


Alisema kuwa leo katika mkutano wake na waandishi wa habari ataeleza yote yaliyotokea na hatua atakazochukua, kwa kuwa yeye ni kiongozi wa juu wa chama.


Hata hivyo, alieleza kwamba bado anashauriana na wanasheria wake kuona kama anaweza kuwachukulia hatua waliompinga.

No comments:

Post a Comment