Monday, August 5, 2013

MAREKANI YAFUNGA BALOZI ZAKE AFRIKA KASKAZINI


Marekani imesema kuwa itafunga balozi zake kadhaa Kaskazini mwa Afrika na Mashariki ya kati hadi Jumamosi wiki ijayo kwa sababu ya hofu ya kushambuliwa na makundi ya wapiganaji wa kiisilamu.Balozi 21 za Marekani na ofisi zake zilifungwa Jumapili.

Uingereza ilisema kuwa Ubalozi wake nchini Yemen utasalia kufungwa hadi mwishoni kwa sherehe za siku kuu ya IDD siku ya Alhamisi na kufunguliwa siku ya Jumanne.Wizara ya mambo ya nje ya Marekani ilisema kuwa kufungwa kwa balozi hizo ni kutokana na serikali kuchukua tahadhari kubwa na wala sio jibu lake kwa tisho jipya la mashambulizi.
Wakati huohuo, balozi za Marekani katika miji ya Algiers, Kabul na Baghdad ni miongoni mwa zile zitakazofungwa na kutarajiwa kufunguliwa Jumatatu wiki ijayo.

Lakini duru za kidiplomasia katika miji ya Abu Dhabi, Amman, Cairo, Riyadh, Dhahran, Jeddah, Doha, Dubai, Kuwait, Manama, Muscat, Sanaa na Tripoli zinasema kuwa
balozi zitasalia kufungwa hadi Jumamosi.

Wizara ya mambo ya nje ya Marekani pia iliongeza kuwa balozi zake katika miji ya Antananarivo, Bujumbura, Djibouti, Khartoum, Kigali na Port Louis pia zitafungwa . Idadi ya balozi za Marekani zitakazofungwa kwa ujumla wiki hii ni 19.

Wizara hiyo ilisema kuwa uwezekano wa balozi hizo kushambuliwa ni kubwa sana hususan Mashariki ya kati na Afrika ya Kaskazini.

Hatua ya kufungwa kwa balozi hizo imekuja baada ya kile Marekani kusema ilinasa ujumbe kutoka kwa kundi la wapiganaji wa kiisilamu la al-Qaeda.

Inasemekana kuwa ujumbe huo ulikuwa kati ya viongozi wawili wakuu wa Al Qaeeda wakipanga mashambulizi.

Onyo hilo pia limetoa tahadhari kwa raia wa Marekani kuwa waangalifu kuhusu tisho la makundi ya wapiganaji kufanya mashambulizi dhidi ya mifumo ya usafiri wa umma pamoja na maeneo mengine ya kitalii.

No comments:

Post a Comment