Wednesday, August 14, 2013

WAFUASI WA MORSI WATAWANYWA MISRI



Polisi nchini Misri, wametumia gesi ya kutoa machozi kuwatawanya waandamanaji wanaomuunga mkono rais aliyeondolewa mamlakani Mohammed Morsi wakati wa maandamano yao mjini Cairo.Vikosi vya usalama viliingilia maandamano hayo baada ya wafuasi wa Morsi kukabiliana na mahasimu wao wa kisiasa.

Morsi aliondolewa mamlakani na viongozi wa jeshi mwezi Julai kufuatia maandamano makubwa sana.Walioshuhudia vurugu hizo walirushiana mawe na chupa huku watoto na wanawake wakikimbilia usalama wao.Tangu hapo jeshi limeweka serikali ya mpito.

Wafuasi wa Morsi aliyeingia mamlakani baada ya vuguvugu la kiisilamu la Brotherhood kushinda uchaguzi wa rais, wanakataa kukubali serikali mpya ya mpito wakisisitiza kuwa lazima rais wao arejeshwe mamlakani. Vurugu za Jumanne zilianza wakati wafuasi wa Morsi, walipotembea hadi sehemu moja ya Cairo ambako watu wengi wanapinga vuguvugu la Muslim Brotherhood.

Waandamanaji hao walijaribu kuingia katika ofisi za wizara moja ingawa polisi waliwalazimisha kuondoka kwa nguvu.Wakaazi wa eneo hilo walianza kuwakejeli waandamanaji na hapo ndipo polisi walipoingilia mzozo huo.Mamilioni ya wamisri waliandamana kumtaka Morsi aondolewe mamlakani ingawa wadadisi wanasema kuwa kuondolewa kwake kunaonekana kuzorotesha migawanyiko ya kisiasa iliyoko kwa sasa.

Wafuasi wake wamekuwa wakipiga kambi mjini Cairo wakitaka arejeshwe mamlakani. Maafisa wa usalama walitishia kuondoa mahema waliyoweka wafuasi wa Morsi ambako wamekuwa wakipiga kambi lakini wakabatili uamuzi wao baada ya kuamua kuuakhirisha.

No comments:

Post a Comment