Tuesday, August 20, 2013

SERIKALI YATOA TAKWIMU WAFUNGWA DAWA ZA KULEVYA

SERIKALI imetoa takwimu za mahabusi waliohukumiwa kwa kesi ya dawa za kulevya ambapo takwimu hiyo inaonyesha jumla ya watu 10 wamehukumiwa kwa kipindi cha mwaka 2010,2012.

Hayo yamesemwa na Msemaji Mkuu wa Serikali ambaye ni Mkurugenzi wa Idara ya Habari Maelezo Assah Mwambene leo jijini Dar es salaam alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari katika ukumbi wa Idara hiyo.


Alisema kuwa jumla ya  washitakiwa wanne walihukumiwa kifungo cha maisha jela Mahakama Kuu mkoani Mtwara baada ya kupatikana na hatia ya kukutwa na kilo nne za dawa za kulevya aina ya heroin Mwaka 2010.

Mwaka 2012 Mahakama Kuu Mkoani Tanga iliwahukumu washitakiwa 5 kifungo cha miaka 25 jela na kulipa faini ya TSh. 1,438,364,000/= kila mmoja baada ya kupatikana na hatia ya kusafirisha kilo 92.2 za dawa za kulevya aina ya heroin. Pamoja na hukumu hiyo, mahakama iliamuru utaifishaji wa magari mawili yaliyotumiwa kusafirisha dawa hizo.

Mwaka 2012 Mahakama Kuu ilitoa hukumu ya miaka 20 jela kwa mshtakiwa mmoja aliyekamatwa na kilo 3 za dawa za kulevya aina ya heroin mkoani Kilimanjaro.

Aliongezea kuwa “Kwa yeyote aliyekuwa anafikiria kufanya biashara ya dawa za kulevya ajue muda wake umekwisha” alisema Mwambene.
Mwambene alisema kuwa tatizo hili litakuwa historia  kwani ulinzi umeimarishwa, hivyo ametoa rai kwa
mtu yeyote mwenye  nia ya kufanya biashara hiyo aache mara moja.

Mkurugenzi huyo alisisitiza kuwa Serikali imeweka jitihada kubwa ya kutoa elimu kwa watumiaji na waathirika wa dawa za kuelevya ili waweze kubadili tabia zao za kutumia dawa hizo na kuwa watu wema katika jamii.



No comments:

Post a Comment