Friday, August 2, 2013

WASHUKIWA WA UGAIDI KULIPWA FIDIA KENYA



Mahakama nchini Kenya, imeamuru waathiriwa kumi na moja waliohamishwa kinyume na sheria kwa madai ya kuwa washukiwa wa ugaidi walipwe fidia, Walikuwa sehemu ya idadi kubwa zaidi ya washukiwa wa ugaidi waliohamishiswa nchi ya kigeni kinyume na sheria.

Mahakama kwa hivyo imeamuru serikali ya Kenya kuwalipa fidia ya kima cha dola 460,000 waathiriwa wa kitendo hicho.Washukiwa hao walikamatwa mwaka 2007 na kuhamishiwa hadi Somalia na wengine wakipelekwa Ethiopia ili kuhojiwa na mashirika ya kijasusi ikiwemo FBI na CIA.Waathiriwa hao walikuwa miongoni wa washukiwa zaidi ya 100 wa ugaidi waliozuiliwa nchini Ethiopia.

Waathiriwa hao wakiwemo wakenya wanane na raia wawili wa Tanzania pamoja na raia mmoja wa Rwanda, walikamatwa katika ufuo wa bahari nchini Kenya na maafisa wa usalama kabla ya kupelekwa kwa lazima nchini Somalia na hatimaye Ethiopia.

Wakati wakiwa nchini Ethiopia, waathiriwa wanasema kuwa waliteswa na kuhojiwa na mashirika kadhaa ya kijasusi ikwemo FBI na CIA.

Ingawa hii ni mara ya kwanza kwa mahakama ya Kenya kuamuru washukiwa wa ugaidi wasio na hatia kulipwa fidia, washukiwa hao kumi na moja hawajafurahishwa na walivyotendewa.

Katika uamuzi wake, mahakama kuu ilipata ushahidi kuwa wahsukiwa hao waliteswa huku haki zai za kikatiba zikikiukwa kwa kupelekwa nje ya nchi kwa nguvu.

Hata hivyo mahakama imeondolea lawama mashirika ya ndege ambayo yalitoa huduma ya kupelekwa kwa washukiwa hao katika nchi ya kigeni.

No comments:

Post a Comment