Wednesday, September 25, 2013

MWANAMKE AONGOZA SHAMBULIZI LA KIGAIDI


Huku mapambano yakiwa yamepamba moto, anayedaiwa kuwa Kiongozi wa kundi la magaidi lililovamia jengo la kibiashara la Westgate, Samantha Lewthwaite inadhaniwa kuwa ameuawa. Lewthwaite, ambaye anaitwa kwa jina la utani la ‘Mjane Mweupe’ anadaiwa kuongoza shambulizi hilo lililosababisha vifo vya watu 62 na kujeruhi wengine 170 mjini Nairobi.

Kwa mujibu wa gazeti la Daily Mail la Uingereza, mwanamke huyo inasemekana aliuawa juzi usiku na wanajeshi wa Kenya wanaoshirikiana na maofisa wa Shirika la Ujasusi la Israel (Mossad) na wale wa Shirika la Upelelezi la Marekani (FBI).

Gazeti hilo lilieleza kuwa mwanamke huyo ambaye ni mjane wa mlipuaji wa kujitoa muhanga, Jermaine Lindsay, aliuawa pamoja na magaidi wengine watatu. Kitendo cha kukutwa kwa mwanamke aliyevalia hijab ndicho kilichowafanya maofisa wa usalama kuamini kuwa mwanamke huyo ameuawa.


Hata hivyo, viongozi wa usalama wa Kenya hawakutaka kuingia kwa undani juu ya taarifa za kifo cha Lewthwaite. Milio ya bunduki na mabomu vilisikika siku nzima ya jana lakini vyanzo mbalimbali vya polisi vilisema kuwa operesheni hiyo ilikuwa inaendelea vizuri na havikutaka kuzungumzia suala la mwanamke huyo. Polisi wa Kenya wamekuwa na kazi ya kutegua mabomu, ambayo yametegwa ndani ya jengo hilo ambalo magaidi wamejichimbia.

“Tuna kazi ya kutegua mabomu yaliyotegwa na magaidi ili tuweze kuwafikia na kuwakamata,” ilisema taarifa ya Jeshi la Polisi wa Kenya kupitia Mtandao wa Twitter. Waziri wa Kenya aibua mapya Katika mahojiano na Kituo cha Televisheni cha Al-Jazeera, Waziri wa Mambo ya Nje wa Kenya, Amina Mohamed alikiri kuwa shambulizi hilo liliongozwa na mwanamke huyo wa Uingereza.

No comments:

Post a Comment