Wednesday, September 4, 2013

PUTIN AMEONYA MAREKANI

Rais wa Urusi Vladimir Putin, ameonya Marekani na nchi za Magharibi dhidi ya kushambulia Syria.Alisema kuwa hatua zozote za kijeshi dhidi ya Syria itakuwa ni uvamizi. Lakini kwenye mahojiano na shirika la habari la Associated Press, kabla ya mkutano wa wiki hii wa G-Twenty mjini St Petersburg, bwana Putin alisema kuwa huenda akaunga mkono azimio la Umoja wa Mataifa ikiwa kuna thibitisho kuwa silaha za kemikali zilitumiwa dhidi ya raia.Rais wa Marekani Barack Obama ametoa wito wa kuchukua hatua za kijeshi dhidi ya Syria baada ya kusema kuwa kuna thibitisho kuwa rais Assad ametumia silaha za kemikali dhidi ya wananchi wake.

Putin pia alipuuza wasiwasi kuwa wanariadha au mashabiki wataadhibiwa ikiwa watatoa matamshi yatakayoonekana kuwa propaganda kuhusu mapenzi ya jinsia moja wakati wa michezo ya olimpiki itakayofanyika nchini humo.

Wakati huohuo , maseneta nchini Marekani wameridhia mswada wa azimio linalompa idhini Rais Barack Obama kutekeleza shambulio la kijeshi dhidi ya Syria. Mswada huo utapigiwa kura wiki ijayo.

Awali Waziri wa mambo ya nchi za nje wa Marekani John Kerry alifika mbele ya Baraza la Senate ambapo alitoa onyo kwa maseneta wa Marekani kabla ya mdahalo wao kuhusu Syria unaotarajiwa kufanyika wiki ijayo kwamba, hawapaswi kushindwa kutoa jibu la kile alichokitaja kuwa ni matumizi ya silaha za kemikali ambayo hayawezi kukanushwa yaliyofanywa na Rais Assad kwa watu wake mwenyewe .

Naye Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon amesema kuwa ikiwa itathibitishwa kwamba silaha za sumu ya kemikali zilitumiwa nchini Syria , baraza la usalama la Umoja wa Mataifa lazima liungane na kuchukua hatua.

No comments:

Post a Comment