Wednesday, September 18, 2013

SERIKALI KUTOA BARUA KWA BALOZI WA CHINA


Dar es Salaam. Serikali imesema mabalozi wanaowakilisha nchi zao nchini wanapaswa kutambua kuwa, wanawajibika kuheshimu Mkataba wa Kimataifa wa Vienna unaoainisha taratibu za diplomasia. Pia, inasema inajiandaa kumwandikia barua Balozi wa China nchini, Lu Younqing kutokana na hatua yake ya kujihusisha na mambo ya siasa.

Wiki iliyopita, Balozi Lu alijitokeza kwenye mkutano wa hadhara wa CCM uliofanyika mkoani Shinyanga, huku akiwa amevalia moja ya sare za chama hicho, hatua ambayo imezusha mjadala miongoni mwa vyama vya siasa na wachunguzi wa mambo ya kidiplomasia. Akizungumzia kitendo hicho jana, Naibu Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Mahadhi Juma Maalim, alisema Serikali inajiandaa kumwandikia barua ya kumkumbusha wajibu wake na kwamba itafanya hivyo baada ya kukusanya taarifa zake.

Hata hivyo, Mahadhi alisema Tanzania na China zitaendelea kuwa marafiki wanaoshirikiana kwenye nyanja mbalimbali kwa shabaha ya kuwaletea maendeleo wananchi wake. “Hizi taarifa za balozi kuwa kwenye mkutano wa CCM nami zimezisikia na kuziona kwenye vyombo vya habari, tunachokifanya sasa wataalamu wetu wanaendelea kuzifanyia kazi, baadaye tutamwandikia barua kumkumbusha wajibu wake,” alisema.
Alisema siyo vyema kwa mabalozi kushiriki mambo ya kisiasa, kwani kufanya hivyo ni kwenda kinyume na Mkataba wa Vienna ambao ndiyo unaotoa mwongozo. Pia, Mahadhi aliasa vyama vya siasa kutoachia majukwaa yao yakitumiwa na wanadiplomasia, akieleza kuwa navyo vinawajibika kuheshimu mkataba huo.
Alisema iwapo pande zote zitaheshimu mkataba huo, hakutakuwa na kurushiana lawama.

No comments:

Post a Comment