Friday, September 27, 2013

NGASSA KUWALIPA SIMBA MWENYEWE


Mshambuliaji wa Yanga na timu ya Taifa (Taifa Stars), Mrisho Ngassa ameamua kulipa mwenyewe deni lake la Sh45 milioni anazotakiwa kuilipa klabu ya Simba baada ya kuhukumiwa na Shirikisho la Soka nchini (TFF).

Awali Ngassa alikuwa ameweka ‘ngumu’ kulipa fedha hizo na kuzua tafrani kwa mashabiki na wanachama wa Yanga kuhusiana na adhabu yake ya kulipa fidia iliyotolewa na Kamati ya Sheria, Maadili na Hadhi ya Wachezaji ya TFF.

Kamati hiyo ilimfungia Ngassa kucheza mechi sita, adhabu ambayo amekwisha itumikia na kilichobakia sasa ni kulipa fedha hizo ili aweze kucheza mechi za Ligi Kuu ya Tanzania Bara.

Pamoja na Ngassa kuonyesha juhudi kubwa mazoezini, sakata la ulipaji wa fedha hizo lilizua tafrani nyingine huku uongozi ukitaka kulipa fedha hizo, lakini kwa masharti ya kuongeza mkataba mwingine.

Hali hiyo ilizua maswali mengi kutokana na ukweli kuwa muda wa kuingia mkataba kwa mujibu wa taratibu za TFF ulikuwa umekwisha na suala hilo lingeweza kufanikiwa wakati wa dirisha dogo la usajili.

Baada ya kukaa kimya cha muda mrefu, Ngassa ameamua kutangaza waziwazi kuwa atalipa fedha hizo alizochukua kutoka Simba na faini ambayo Kamati ya Sheria, Maadili na Hadhi ya Wachezaji iliyoamua. Kamati hiyo ilimtaka Ngassa kulipa fidia ya asilimia 50 ya fedha Sh30 milioni alizochukua kutoka Simba.

Ngassa alisema kuwa ameamua kutoa fedha hizo kutoka katika vitega uchumi vyake na amefanya hivyo kwa sababu suala hilo linamhusu yeye huku klabu yake ya Yanga ikiadhibiwa pasipo sababu.

“Nina magari na biashara zangu, nitalipa fedha hizo na nitarejea Jumamosi kucheza mechi yangu ya kwanza ya Ligi Kuu ya Tanzania Bara dhidi ya Ruvu Shooting, mpira ni kazi yangu na hili nimelifanya kutokana na mapenzi yangu ya dhati na Yanga,” alisema Ngassa.

Alisema kuwa hajisikii vizuri kukaa nje ya uwanja huku akiamini kuwa kipaji chake kinapotea. “Nimekaa nje, sikuwa na raha, sasa narejea kwa nguvu zote ili kuendeleza gurudumu la Yanga, mawazo yangu ya kucheza nje ya nchi kwa sasa nimeyafuta na hasa baada ya kupata ushauri kutoka kwa marafiki zangu, nawaomba radhi mashabiki na wanachama wa Yanga,” alisema Ngassa.

No comments:

Post a Comment